

Dodoma. Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya imezindua rasmi kampeni ya INSPIRE TO LEAD yenye lengo la kubadilisha fikra na mitazamo ya jamii kuhusu usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika nafasi za uongozi.
Uzinduzi huo umefanyika leo, Juni 25, 2025, jijini Dodoma na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo maafisa habari kutoka wizara mbalimbali, wawakilishi wa mashirika ya kiraia, wanafunzi na wanaharakati wa masuala ya kijinsia.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima amesema kampeni hiyo inalenga pia kuongeza hali ya kujiamini kwa wanawake na wasichana pamoja na kuwawezesha kushiriki katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM).
“Hatuna budi kushirikiana kwa pamoja kwani kampeni hii si ya Wizara moja au Serikali pekee, ndiyo maana tumewaalika wadau mbalimbali ili kwa pamoja tujenge jamii yenye usawa wa kijinsia,” amesema Dk. Gwajima.
Ameeleza kuwa kupitia kampeni hiyo, Serikali inatarajia kuona matokeo chanya katika kipindi cha miaka michache ijayo ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa idadi ya wanawake katika nafasi za uongozi, hususan katika sekta ambazo awali zimekuwa zikitawaliwa na wanaume kama vile uhandisi, madini na urubani.
“Uelewa wa jamii kuhusu usawa wa kijinsia utaongezeka, vitendo vya ukatili vitaendelea kupungua na idadi ya wasichana wanaojiunga na masomo ya STEM itaongezeka,” amesema.
Waziri Gwajima ametoa wito kwa washiriki wote wa kampeni hiyo kuhakikisha ujumbe unawafikia walengwa kwa usahihi ili kuijenga jamii yenye uelewa, wanawake jasiri na wasichana wenye uthubutu wa kuchukua mwelekeo wa sayansi na teknolojia kwa maendeleo ya taifa.
Kampeni ya INSPIRE TO LEAD ni sehemu ya jitihada za Serikali na wadau wa maendeleo katika kufikia usawa wa kijinsia na kujenga jamii jumuishi yenye fursa sawa kwa wote.
Waziri Mhagama ametoa Agizo Vituo Vyote Vinavyotoa Huduma za Afya Viweke Wazi Mikataba Kwa Wateja.
Wenye malori watakiwa kuweka vifaa vya usalama
Mavunde Akabidhi Jengo la kupumzikia Wananchi Hospitali ya Rufaa ya Dodoma
Waziri Mhagama ametoa Agizo Vituo Vyote Vinavyotoa Huduma za Afya Viweke Wazi Mikataba Kwa Wateja
HAKUNA MWENYE MAMLAKA YA KUZUIA UCHAGUZI:VIJANA CCM.
GRAND BUNGE BONANZA KUFANYIKA JUNI 21 2025 HUKU MGENI RASMI AKITARAJIWA KUWA RAIS SAMIA.
CDE SALUM ATANGAZA NIA KUGOMBEA UBUNGE JIMBO LA KAHAMA MJINI.
KIHENZILE:WIKI YA UTUMISHI WA UMMA NI FURSA MUHIMU KWA WANANCHI
MOI YASEMA WAGONJWA WENGI WANAOWAHUDUMIA WANA MATATIZO SUGU.
PPAA yatoa elimu matumizi ya Moduli Wiki ya Utumishi wa Umma