

Benki ya Ushirika (Coop Benki), kwa kushirikiana na Mfuko wa Pembejeo wa Kilimo (AGITIF), imetoa mkopo wa jumla ya shilingi bilioni 8.5 kwa vijana na wanachama wa vyama vya ushirika kutoka maeneo mbalimbali nchini, ikiwa ni juhudi za kuongeza tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo.
Akizungumza katika Maonesho ya Wakulima na Wafugaji (Nanenane) yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa Coop Benki, Bw. Godfrey Ng’urah, alisema mkopo huo utatolewa kupitia vyama vya ushirika ili kuwafikia wakulima wengi zaidi, wakiwemo vijana na wanawake
“Benki ya Ushirika, kwa kushirikiana na AGITIF, inatoa mikopo hii kwa dhamira ya kuchochea kilimo chenye tija na kuwakwamua wakulima kiuchumi. Leo tunatoa mkopo wa shilingi bilioni 8.5 kama sehemu ya juhudi hizo,” alisema Bw. Ng’urah.
Alieleza kuwa AGITIF, ambao ulianzishwa mwaka 1994, umekuwa ukitoa huduma za kifedha kwa watu binafsi, taasisi za kifedha na makundi maalum katika sekta ya kilimo. Mfuko huo umeweka kipaumbele kwa vijana walio na umri chini ya miaka 40 pamoja na wanawake
“Hadi sasa, AGITIF imeshatoa zaidi ya shilingi bilioni 94 ambazo zimeelekezwa katika miradi ya umwagiliaji na kuongeza uzalishaji mashambani,” aliongeza.
Bw. Ng’urah alibainisha kuwa Coop Benki itasimamia utoaji wa mikopo hiyo kama wakala rasmi, huku lengo kuu likiwa ni kuwafikia wakulima wa mijini na vijijini kupitia vyama vya ushirika na matawi ya benki hiyo nchini kote.
Akizungumza kwa niaba ya Wizara ya Kilimo, Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Dkt. Hussein Mohamed Omar, aliwataka wakulima kuhakikisha wanarejesha mikopo kwa wakati ili wengine nao wanufaike
“Mkopo huu ni wa mzunguko. Hivyo ni muhimu urejeshwe kwa wakati ili kuwezesha wakulima wengine kunufaika katika mzunguko unaofuata,” alisisitiza Dkt. Omar.
Mpango huu unakwenda sambamba na juhudi za Serikali za kuimarisha sekta ya kilimo kupitia upatikanaji wa mitaji nafuu kwa wakulima, kwa lengo la kuongeza tija, kipato cha kaya, na kuchochea ajira vijijini.
Maonesho haya kwa mwaka 2025 yamebeba kauli mbiu “Chagua Viongozi Bora kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi 2025”. Maonesho ya NaneNane Kitaifa yalifunguliwa rasmi tarehe 1 Agosti, 2025 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mapango. Maonesho hayo yalianza tarehe 1 hadi 8 Agosti 2025.
KIBONDE WA CHAMA CHA MAKINI ACHUKUA FOMU ZA KUWANIA URAIS INEC
KADEGE WA CHAMA CHA UPDP ACHUKUA FOMU ZA URAIS
INEC YAMKABIDHI FOMU ZA UTEUZI MGOMBEA URAIS WA CHAMA CHA NLD DOYO HASSAN DOYO
NCHIMBI AKIPOKEA BARAKA ZA MAMA YAKE MZAZI
MGOMBEA KITI CHA URAIS KWA TIKETI YA CHAMA CHA NRA ACHUKUA FOMU TUME
VIONGOZI WA DINI WAASWA KUSHUGHULIKIA MIGOGORO YAO YA NDANI PASIPO KUZUA TAHARUKI ILI KULINDA AMANI YA NCHI.
Coop Bank Imejipanga Kutoa Huduma Maalum kwa Washiriki wa Maonesho ya NaneNane.
CUF KUPITISHA WAGOMBEA URAIS AGOSTI 9 MAJINA YATAJWA.
TICEZA Kuwapa Watanzania Maeneo Bure Kujenga Viwanda
SENYAMULE AIPONGEZA DIB UTOAJI WA ELIMU KWENYE MAONESHO NANENANE.