

Mkurugenzi wa Masoko wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Bw. Ernest Mwamwaja amesema Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia bodi hiyo itaendelea kuitangaza Tanzania kwa nguvu zote katika maonesho ya Uchumi na Biashara maarufu kama Expo Osaka 2025 yanayofanyika nchini Japan.
Bwana Mwamwaja ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumzia kuhusu mwenendo wa ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo yanayoratibiwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara-TANTRADE yaliyoanza Aprili 13 mwaka huu na yanatarajiwa kuendelea kwa muda wa miezi 6 ambapo yatamalizika mwezi Oktoba mwaka huu.
Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa hadi sasa Tanzania imefanikiwa kuvutia watembeleaji wengi katika banda lake na watu wanaopata taarifa kuhusu vivutio vilivyopo wameonesha nia ya kuvitembelea.
“Tunafarijika kuona kwamba idadi ya watembeleaji katika banda letu ni kubwa na wengi wao wanaonesha dhamira ya dhati ya kutaka kufika Tanzania baada ya kunadi vivutio vyetu, kwetu sisi kama wizara haya ni mafanikio makubwa”,alisema Bw. Mwamwaja.
Katika wiki hii ya Utalii iliyoanza tarehe 25 Aprili 2025, ambayo kwa upande wa Tanzania ilizinduliwa na Balozi wa Tanzania nchini Japan, Mhe. Baraka Luvanda, Tanzania imeitumia wiki hiyo kutangaza fursa za utalii zilizopo.
Taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii zikiwemo Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) yameendela kutumia fursa hiyo kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika maeneo yao.
Akizungumzia ushiriki katika maonesho hayo Naibu Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Bw. Massana Mwishawa ameelezea kuwa shirika hilo limetangaza maeneo ya uwekezaji hasa katika huduma za malazi na shughuli za utalii.
Kwa upande wake, Afisa Uhifadhi Mkuu upande wa masoko kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bw Michael Makombe amesema NCAA imekuwa ikitumia fursa hiyo kuwakaribisha wageni kutembelea hifadhi hiyo na kujionea fursa mbalimbali zilizopo.
Akizungumzia ushiriki wa TAWA katika maonesho hayo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa mamlaka hiyo Bi. Lilian Wawa amesema kutoka pamoja na kunadi utalii, OSAKA EXPO 2025 inatumika kushawishi uwekezaji wa Kampuni za kimataifa katika mazao ya utalii wa Uwindaji na wa picha.
Maonesho ya Osaka EXPO yanayoendelea nchini Japan yanatarajiwa kutembelewa na wageni wasiopungua milioni 28 waoneshaji kutoka zaidi ya nchi 160 duniani wanashiriki.
EVANCE KAMENGE AJITOLEA KUSAIDIA JAMII KAGERA
SERIKALI KUTEKELEZA MFUKO WA UBUNIFU WA SAMIA “SAMIA INNOVATION FUND” WENYE THAMANI YA BIL 2.3
SERIKALI YAENDELEA KUTOA MAFUNZO KWA WALIMU 70,657 UTEKELEZAJI MITAALA ILIYOBORESHWA, YAANZA MAPITIO SHERIA YA ELIMU
DKT. DORIYE AVISHA VYEO VYA KIJESHI MAAFISA 145 NA ASKARI 476 WA NCAA NA KUSISITIZA UCHAPAKAZI, NIDHAMU, MAADILI NA UZALENDO KATIKA ULINZI WA RASILIMALI.
WAHUKUMIWA MIAKA 20 GEREZANI KWA KUHUJUMU MRADI WA ETDCO
Ibraah Afunguka: "Nilifukuzwa Konde Gang na Harmonize"
Watu Wenye Ulemavu Waomba Kuangaliwa kwa Jicho la Kipekee Katika Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.
Sekta ya Uvuvi imetoa ajira ya Moja Kwa Moja Kwa Wavuvi 201,661
BODI YA ITHIBATI YATAMBULISHWA RASMI BUNGENI
SERIKALI Imeendelea Kujenga na Kuboresha Miundombinu ya Viwanja vya Ndege